Mambo ya Haramu yanayofanyika Saloon katika kazi ya kinyozi
Tunaendeleaa....
Tunaendeleaa....
3. Kunyoa Nyusi
Naam vilevile baadhi ya vinyozi hukata vijana wa kiume nyusi. Vijana wanaoiga wanamuziki na wachezaji mpira. Kijana akiona mcheza mpira maarufu kaweka mistari kwenye nyusi zake naye aenda kumuiga.
Vinyozi wanapoendewa na vijana kama hao, wao wanaona “pesa mbele dini baadae” wanatekeleza wateja wao wanavyotaka.
Mteja akikaa tu kwenye kiti, akiamrisha afanyiwe mtindo wowote, basi naye kinyozi asiyejitambua ambaye ima hajui chochote kuhusu mafunzo ya dini yake na hataki kujishughulisha kujua, au anajua lakini pesa imegeuka kuwa ndio dini yake, basi hutekeleza yale mteja anayoyataka tena wakati mwengine kwa fakhari aonekane mnyoaji mahiri na hakuna mtindo unaomshinda!
Kutoka kwa 'Abdullah bin Mas'uwd (Radhwiya Allahu 'anhu) kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((Allaah Amewalaani watu wenye kuwachanja wenzao (tattoo) na wenye kuchanjwa, na wenye kuwanyoa wenzao nyusi na wenye kunyolewa na wenye kuchonga meno yao (kama kufanya mwanya) kwa ajili ya kujipamba kubadilisha maumbile ya Allaah) [Al-Bukhaariy na Muslim]
Kitendo cha unyoaji nyusi japo kwa mazoea kinafanywa na wanawake, na laana hizo zinawaendea wanaofanya na kuwafanyia wenzao hivyo, lakini kwa mwanamme laana inakuwa ni kali zaidi kwani kunapatikana maharamisho mawili ndani yake; ya kunyoa nyusi na ya kujifanananisha na wanawake.
Eee mja ikiwa unamuogopa Mola wako na Siku ya Mwisho na adhabu ya Moto, jiepushe na matamanio hayo machafu ya kipumbavu ambayo hayakunufaishi chochote wala kukuongezea zaidi ya kumuasi Mola wako na kujipalilia adhabu Yake isiyostahamilika.
4. Vikao vya Kusengenya na Umbea
Mara nyingi katika saluni za kunyolea, kunakuwa na mazungumzo ya kusengenya na umbea umbea mwingi. Hususan saluni hizi ambazo tunazizungumzia hapa zenye sifa zisizo za Kiislamu.
Si rahisi kukuta vinyozi wengi kufanya kazi zao huku wanamtaja Allaah na kumsabbih au kumhimidi au kufanya istighfaar au kwa uchache kufanya kazi kimya kimya. Utakuta ni wazungumzaji na wenye soga nyingi za kipuuzi wakidhani ndio kumfurahisha mteja au kumchangamsha. Na ikiwa mteja si mtu wa upuuzi na hapendi usengenyaji au umbea au hawajamzoea, basi wao kwa wao huendeleza mazungumzo ya kipuuzi au ya kidunia.
Ni nadra sana kukuta kuna mazungumzo ya dini ya kufaidishana. Hata yakiwepo mazungumzo ya dini, basi ni yale hasi na si chanya. Ima watakosoa mambo ya dini ambayo wao hawako tayari kuyatekeleza kama haya tunayoyataja humu ndani yasiyofaa wao kuyafanya, au utawakuta wanasengenya watu wanaojishughulisha na Dini na Da’wah.
Katika mifano hai ambayo iko tele, lakini tukigusa mifano miwili mitatu, kuna baadhi ya saluni ndio vituo vikubwa vya watu wapinzani wa dini, na wale wasioswali, wale mabingwa wa kusengenya na umbea na mipasho, na hata wale maadui wakubwa wa dini kama wale watukanao Maswahaba.
Katika saluni za moja ya miji ya Ulaya, kuna adui mmoja wa dini ambaye saluni hiyo ni kituo chake kikubwa cha kupotezea wakati na kupotosha itikadi za Waislamu. Waislamu hao wenye saluni ni watu wanaojinasibisha na Usunni lakini wasiotaka kujishughulisha na elimu na wajuaji wasiotaka kufunzwa.
Adui huyo maarufu kazi yake ni kwenda kuwatia hao wenye saluni na wateja wao, mashaka katika dini yao kama kuwatia kasoro Maswahaba na kuwatukana, pia kuhalalisha haramu kama ribaa za benki akiwakinaisha hao wasiojitambua huku akiwachezea kwa kuzipindua Aayah na kuzibadilisha maana, vilevile kuhalalisha ndoa ya muda, kuhalalisha unyoaji ndevu kwani yeye mwenyewe kajipamba kwa sifa ya uke, kuhalalisha mavazi yaliyokatazwa uvaaji wake kama vile mwanamme kuburuza nguo n.k, kwani yeye mwenyewe nguo zake zinafagia barabara na hana alama ya kutambulisha Uislamu wake si kwa dhahiri wala kimatendo! Na zaidi adui huyo huwatukana Wanachuoni wa haki na hata Walinganiaji wa dini na kuwabeza kwa sababu hawakubaliani na itikadi yake ya kikafiri.
Na maskini hao wajuaji wenye masaluni hayo wasiojua chochote zaidi ya kusengenya, huwa wakimsikiliza adui huyo muovu na kuvutika naye kwa sababu huwa anawapeleka kule kule matamanio yao yanapotaka!
Jambo la kushangaza, adui huyo wa dini mwenye chuki na Maswahaba kama ilivyo dini yao ambayo inajinasibisha na Uislamu ilhali Uislamu uko mbali nao, anashinda masaa mengi kwenye saluni hiyo kupoteza watu na akionekana kuzungumzia mambo ya dini lakini haonekani kuswali na nyakati zote za Swalaah zinamkuta akipiga domo hapo kuwapoteza wajinga wajuaji wasiotaka kujishughulisha na elimu.
Lakini hao wenye saluni, hawana hata ile akili ndogo ya kujiuliza mbona huyu kiumbe anajifanya kuzungumzia mambo ya dini na kuyachambua lakini hata haendi kuswali???
Huo ni mfano mmoja wa mabalaa yanayopatikana kwenye saluni za Waislamu wasiojitambua na wasiotaka kufuata mafunzo ya dini yao, achilia mbali mazungumzo ya kutiana mashaka mashaka katika masaail mbalimbali ya dini wakibeza Sunnah za Mjumbe wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na kufanyia maamrisho ya dini istihzai. Wakibeza mavazi, madhahiri (mionekano) ya watu wanaofuata Sunnah, na hata wakibeza mafunzo mbalimbali ya dini...
Allaah Anasema kuwaelekezea watu sampuli hiyo:
“Na ukiwauliza, bila shaka watasema: “Hakika tulikuwa tunaporoja na tunacheza.” Sema: Je, mlikuwa mnamfanyia istihizai Allaah na Aayaat Zake na Rasuli Wake?
“Msitoe udhuru. Mmekwishakufuru baada ya kuamini kwenu. Tukilisamehe kundi miongoni mwenu, Tutaliadhibu kundi (jingine), kwa kuwa wao walikuwa wahalifu.” [At-Tawbah: 65-66]
Vilevile kunajadiliwa maisha ya watu, hali ya kuwa wao wenyewe wana mabalaa makubwa yasiyoelezeka. Lakini mara nyingi mtu hajioni aibu zake.
Inaendeleaa....USIKOSE TOLEO LINAFUATA MUDA SI MREFU IN SHAA ALLAAH.....
https://ift.tt/2E2MBRE i live islam
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni