
Fadhila Za Nabiy (Swalla Allaahu 'Alayhi Wa Aalihi Wa Sallam)
00-Na Fadhila Za Allaah Juu Yako Daima Ni Adhimu
Allaah ('Azza wa Jalla) Amefadhilisha baadhi ya Manabii juu ya wengine kama Anavyosema:
وَرَبُّكَ أَعْلَمُ بِمَن فِي السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ ۗ وَلَقَدْ فَضَّلْنَا بَعْضَ النَّبِيِّينَ عَلَىٰ بَعْضٍ ۖ وَآتَيْنَا دَاوُودَ زَبُورًا ﴿٥٥﴾
Na Rabb wako Anawajua vilivyo waliomo katika mbingu na ardhi. Na kwa yakini Tumewafadhilisha baadhi ya Manabii juu ya wengineo. Na Tukampa Daawuwd Zabuwr [Al-Israa: 55]
Na Amefadhilisha baadhi ya Rusuli juu ya wengineo kama Anavyosema pia:
تِلْكَ الرُّسُلُ فَضَّلْنَا بَعْضَهُمْ عَلَىٰ بَعْضٍ ۘ مِّنْهُم مَّن كَلَّمَ اللَّـهُ ۖ وَرَفَعَ بَعْضَهُمْ دَرَجَاتٍ ۚ وَآتَيْنَا عِيسَى ابْنَ مَرْيَمَ الْبَيِّنَاتِ وَأَيَّدْنَاهُ بِرُوحِ الْقُدُسِ ۗ
Hao ni Rusuli, Tumewafadhilisha baadhi yao juu ya baadhi. Miongoni mwao kuna aliyesemeshwa na Allaah, na Akawapandisha baadhi yao vyeo. Na Tukampa ‘Iysaa mwana wa Maryam hoja bayana na Tukamtia nguvu kwa Ruwhil-Qudus (Jibriyl (عليه السلام [Al-Baqarah: 253]
Nini Tofauti Ya Rasuli Na Nabiy?
‘Ulamaa wamesema mengi kuhusu tofauti baina ya Rasuli na Nabiy. Wakakubaliana wengi wao kwamba Rasuli ni ambaye ameteremshiwa shariy’ah na akaamrishwa kubalighisha. Ama Nabiy ni ambaye ametumwa na Allaah ('Azza wa Jalla) bila kuteremshiwa shariy’ah mpya naye hutumia shariy’ah ya Rasuli aliyemtangulia.
Shaykhul-Islaam ibn Taymiyyah amesema: “Rasuli ni ambaye aliyetumwa kwa kaumu makafiri waliokanusha. Nabiy ni aliyetumwa kwa Waumini kwa shariy’ah ya Rasuli wa kabla yake awafunze na awahakumu baina yao kama Anavyosema Allaah ('Azza wa Jalla):
إِنَّا أَنزَلْنَا التَّوْرَاةَ فِيهَا هُدًى وَنُورٌ ۚ يَحْكُمُ بِهَا النَّبِيُّونَ الَّذِينَ أَسْلَمُوا لِلَّذِينَ هَادُوا
Hakika Tumeteremsha Tawraat humo mna mwongozo na nuru; ambayo kwayo, Nabiy waliojisalimisha (kwa Allaah), waliwahukumu Mayahudi... [Al-Maaidah: 44]
Kwa ufupi ni kuwa kila Rasuli ni Nabiy lakini si kila Nabiy ni Rasuli. Na ‘Ulamaa wamekubaliana kwamba Rasuli ni bora kuliko Nabiy. Hivyo Rasuli ana daraja kubwa kuliko Nabiy.
Na katika ambao Allaah ('Azza wa Jalla) Amewafadhilisha juu ya wengine ni ambao wanaojulikana kwa Ulul-‘Azmi kama Anavyosema Allaah ('Azza wa Jalla):
وَإِذْ أَخَذْنَا مِنَ النَّبِيِّينَ مِيثَاقَهُمْ وَمِنكَ وَمِن نُّوحٍ وَإِبْرَاهِيمَ وَمُوسَىٰ وَعِيسَى ابْنِ مَرْيَمَ ۖ وَأَخَذْنَا مِنْهُم مِّيثَاقًا غَلِيظًا ﴿٧﴾
Na pale Tulipochukua kutoka kwa Manabii fungamano yao na kutoka kwako, na kutoka kwa Nuwh, na Ibraahiym, na Muwsaa, na ‘Iysaa mwana wa Maryam; na Tukachukua kutoka kwao fungamano gumu. [Al-Ahzaab: 7]
Na Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amefadhilishwa kwa fadhila adhimu na nyingi mno kama Anavyosema Allaah (‘Azza wa Jalla) katika kauli Yake:
وَكَانَ فَضْلُ اللَّـهِ عَلَيْكَ عَظِيمًا ﴿١١٣﴾
Na fadhila za Allaah juu yako daima ni adhimu. [An-Nisaa: 113]
Tutaendelea kutaja fadhila za Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) katika makala zinazofuata.
WabiLLaahi At-Tawfiyq
from Alhidaaya.com http://bit.ly/2EU4FjQ
via IFTTT
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni