Translate

Jumanne, 30 Oktoba 2018

Hukmu ya Ghiyba ( kusengenya )

 Assallaam  Aleykum  WarahmatulLaah  Wabarakatuh

Maana ya Ghiybah:

Kilugha:  Kila kilichokuwa hakipo mbele yako. Na imeitwa Ghiybah kwa kutokuweko anayetajwa wakati anapotajwa na wengine. 

Kishariy’ah: Kumsengenya mtu asiyekuwepo kwa mambo ambayo atachukia kuyasikia. Na maana yake ametujulisha Rasuli wa Allaah  (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alipowauliza Maswahaba:


(( أتدرون ما الغيبة؟))  قالوا: الله ورسوله أعلم؛ قال: (( ذكرك أخاك بما يكره  ...))
((Je mnajua maana ya  Ghiybah?)) Wakasema: Allaah na Rasuli Wake wanajua. Akasema: ((Kumsema ndugu yako anayoyachukia …..))  [Al-Bukhaariy]


Imaam An-Nawawiy amesema kuhusu Ghiybah: "Kumsema mtu nyuma yake kwa yale anayoyachukia."

Akaendelea kusema: "Kumsema mtu kwa anayoyachukia ikiwa yanayohusu mwili wake, au Dini yake, au dunia yake, au nafsi yake, au umbile lake au tabia yake, au mali yake, au wazazi wake, au mtoto wake, au mke wake, au mtumishi wake, au nguo yake, au nyendo (shughuli) zake na mengineyo yote yanayomhusu, ikiwa ni kumsema kwa kauli, au kwa ishara au kukonyeza, hata kama kusema neno la kumkejeli.”
  
Maana nyingine ya Ghiybah ni kama alivyosema Ibn   Taymiyyah (Rahimahu Allaah): "Wengine wanasengenya kwa kauli zao za kustaajabu kama kusema: “Nimeshangazwa na fulani vipi hafanyi kadhaa na kadhaa.” Na wengine wanaosengenya moyoni (kwa niyyah) kwa kunena: “Masikini fulani amenisikitisha anayoyatenda.”

Tofauti Baina ya Ghiybah na Buhtaan:

Buhtaan ni kumzulia mtu jambo lisilokuwa la kweli. Ametubainishia Rasuli wa Allaah   (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) tofauti baina ya Ghiybah na Buhtaan katika Hadiyth ifuatayo:


 عَنْ أَبِي هُرَيْرَةَ رضي الله عنه ، أَنَّ رَسُولَ اللَّهِ صَلَّى اللَّه عَلَيْهِ وَسَلَّمَ قَال:   (( أَتَدْرُونَ مَا الْغِيبَةُ ؟ ))  قَالُوا : اللَّهُ وَرَسُولُهُ أَعْلَمُ ، قَالَ  ((ذِكْرُكَ أَخَاكَ بِمَا يَكْرَهُ )) ، قِيلَ : أَفَرَأَيْتَ إِنْ كَانَ فِي أَخِي مَا أَقُولُ ؟ قَالَ  ((إِنْ كَانَ فِيهِ مَا تَقُولُ فَقَدِ اغْتَبْتَهُ ، وَإِنْ لَمْ يَكُنْ فِيهِ فَقَدْ بَهَتَّهُ))    أخرجه مسلم  
Kutoka kwa Abuu Hurayrah (Radhwiya Allaahu ‘anhu) kwamba aliuuliza Rasuli wa Allaah  (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam): ((Je mnajua maana ya  Ghiybah?))Wakasema: Allaah na Rasuli Wake wanajua. Akasema: ((Ni kumtaja ndugu yako kwa jambo analochukia)). Akaulizwa: Hebu nieleze, iwapo ndugu yangu anayo yale niyasemayo? Akasema: (Ikiwa analo hilo usemalo basi umeshamsengenya, na ikiwa hana hilo usemalo basi umeshamzushia uongo)) [Muslim]

Vile vile Hadiyth ifuatayo inaelezea:


عبد الله بن عمرو أنهم ذكروا عند رسول الله صلى الله عليه وسلم رجلاً فقالوا: لا يأكل حتى يُطعم، ولا يَرحل حتى يُرحل، فقال النبي صلى الله عليه وسلم: ((اغتبتموه)) فقالوا: يا رسول الله: إنما حدثنا بما فيه قال: ((حسبك إذا ذكرت أخاك بما فيه))  المحدثالألباني -  المصدر السلسلة الصحيحة
Kutoka kwa 'Abdullaah bin 'Amru (Radhwiya Allaahu ‘anhu) kwamba walimtaja mtu mmoja mbele ya Rasuli wa Allaah  (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) wakasema: "Hali hadi alishwe, wala haendi hadi apelekwe." Akasema Rasuli wa Allaah  (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) ((Mmemsengenya)).  Wakasema: "Ee Rasuli wa Allaah  wa Allaah, tumehadithia ya kweli aliyonayo." Akasema: ((Inakutosheleza kumsema ndugu yako kwa aliyonayo)) [Al-Albaaniy   katika Silsilatus-Swahiyhah]

 Na kutoka katika Qur-aan Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Anasema:

وَالَّذِينَ يُؤْذُونَ الْمُؤْمِنِينَ وَالْمُؤْمِنَاتِ بِغَيْرِ مَا اكْتَسَبُوا فَقَدِ احْتَمَلُوا بُهْتَانًا وَإِثْمًا مُّبِينًا ﴿٥٨﴾
Na wale wanaowaudhi Waumini wa kiume na Waumini wa kike bila ya kuwa wamechuma kosa, basi kwa yakini wamejibebea usingiziaji mkuu wa dhulma na dhambi bayana. [Al-Ahzaab: 58]  

Vile vile katika kisa cha Ifk (kuzuliwa) Mama wa Waumini 'Aaishah (Radhwiya Allaahu 'anhaa) Anasema Allaah   (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

 وَلَوْلَا إِذْ سَمِعْتُمُوهُ قُلْتُم مَّا يَكُونُ لَنَا أَن نَّتَكَلَّمَ بِهَـٰذَا سُبْحَانَكَ هَـٰذَا بُهْتَانٌ عَظِيمٌ ﴿١٦﴾
Na kwa nini mlipoisikia (kashfa ya kusingiziwa) msiseme: “Haitupasi sisi tuzungumze haya; Subhaanak! (Utakasifu ni Wako) huu ni usingiziaji wa dhulma mkubwa mno!”  [An-Nuwr: 16]    

Uzushi unaweza kuwa kwa Ghiybah  (kumsengenya nyuma yake mtu) au mbele yake. 

Hasan Al-Baswriy kasema: "Ghiybah ni tatu; zote zimo katika Qur-aan. Ghiybah (kusengenya) ifk (usingiziaji, udaku, umbeya) na buhtaan (kusingizia yasiyo kweli).

Ghiybah ni kumsengenya ndugu yako aliyonayo. Ama  Ifk ni kusema unayoyasikia (ya usingiziaji, umbeya) na ama buhtaan ni kusingizia yasiyo kweli."

Ghiybah hakika ni hatari mno kwa Muislamu kwani     ghiybah zinamharibia mtu ‘amali zake na hatimaye akute patupu katika miyzaan yake ya ‘amali njema Siku ya Qiyaamah. Hatari hii ni kwa yeyote yule hata kama mtu ni mswalihina au ni mtendaji  wema kwa wingi!    


Kutunza Ulimi


Kila binaadamu ana Malaika wawili; mmoja kuliani mwake, na kushotoni mwake. Na kazi zao ni kuandika mema ya mtu na maovu yake; ikiwa ni makubwa au madogo hata kama chembe cha hardali basi huandikwa na Malaika hao, hata kama binaadam atatamka neno liwe dogo mno vipi basi litaandikwa. Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

وَلَقَدْ خَلَقْنَا الْإِنسَانَ وَنَعْلَمُ مَا تُوَسْوِسُ بِهِ نَفْسُهُ ۖ وَنَحْنُ أَقْرَبُ إِلَيْهِ مِنْ حَبْلِ الْوَرِيدِ﴿١٦﴾
Na kwa yakini Tumemuumba insani na Tunajua yale yanayowaza nafsi yake, na Sisi Tuko karibu naye kuliko mshipa wa koo.

إِذْ يَتَلَقَّى الْمُتَلَقِّيَانِ عَنِ الْيَمِينِ وَعَنِ الشِّمَالِ قَعِيدٌ﴿١٧﴾
Pale wanapopokea wapokeaji wawili (Malaika) wanaokaa kuliani na kushotoni. 

مَّا يَلْفِظُ مِن قَوْلٍ إِلَّا لَدَيْهِ رَقِيبٌ عَتِيدٌ﴿١٨﴾
Hatamki kauli yeyote isipokuwa anaye mchungaji aliyejitayarisha (kurekodi). [Qaaf: 16-18]

  Hakuna kitakachokosekana kuandikwa na Malaika hao, wala binaadamu hawezi kuwakwepa kwani wao wamewekwa kwa ajili hiyo: Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

وَإِنَّ عَلَيْكُمْ لَحَافِظِينَ ﴿١٠﴾
Na hakika juu yenu bila shaka kuna wenye kuhifadhi (na kuchunga).  


كِرَامًا كَاتِبِينَ ﴿١١﴾
Watukufu wanaoandika (amali).


يَعْلَمُونَ مَا تَفْعَلُونَ ﴿١٢﴾
Wanajua yale myafanyayo. [Al-Infitwaar: 10-12]

Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Ametuumba katika umbo bora kabisa na Amepanga kila kiungo mahali pake panapostahiki. Kwa hikma Yake, Ameviumba viungo viwili muhimu katika mwili wa binaadamu katika sehemu zilizofichika ili vihifadhike visidhihirike nje ya mwili wake. Navyo ni: ulimi na sehemu za siri. Ni viungo ambavyo pindi binaadamu atakapovichunga basi vitampeleka Jannah kama Anavyosema Rasuli wa Allaah  (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam):

 عَنْ سَهْلِ بْنِ سَعْدٍ رضي الله عنه ، عَنْ رَسُولِ اللَّهِ صَلَّى اللَّه عَلَيْهِ وَسَلَّمَ قَالَ: (( مَنْ يَضْمَنْ لِي مَا بَيْنَ لَحْيَيْهِ وَمَا بَيْنَ رِجْلَيْهِ ، أَضْمَنْ لَهُ الْجَنَّةَ))    متفق عليه
Sahl bin Sa'd (Radhwiya Allaahu 'anhu) amesema: Rasuli wa Allaah  (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((Atakayenidhaminia kilichomo baina ya taya zake [yaani ulimi] na kilichomo baina ya miguu yake [yaani tupu au sehemu za siri] nami nitamdhamini Jannah)) [Al-Bukhaariy na Muslim]

Katika Hadiyth nyingine:

عن عقبة بن عامر رضي الله عنه قال : قلت : يا رسول الله ما النجاة ؟ قال: ((مْسِكْ عَلَيْكَ لِسَانَكَ ، وَلْيَسَعْكَ بَيْتُكَ ، وَابْكِ عَلَى خَطِيئَتِكَ)) رواه الترمذي   صححه الألباني في صحيح الترغيب 3331    
'Uqbah bin 'Aamir (Radhwiya Allaahu 'anhu) amesema: "Nilimuuliza Rasuli wa Allaah  (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) "Ee Rasuli wa Allaah, ni kupi kuokoka? Akajibu: ((Uzuie ulimi wako, utosheke na nyumba yako na ulie juu ya dhambi zako)) [At-Tirmidhiy na ameipa daraja ya Swahiyh Al-Albaaniy katika Swahiyh At-Targhiyb (3331)]

 وعَنْ أَبِي هُرَيْرَةَ رَضِي اللَّه عَنْه قَالَ : قَالَ رَسُولُ اللَّهِ صَلَّى اللَّه عَلَيْهِ وَسَلَّمَ :  (( مَنْ كَانَ يُؤْمِنُ بِاللَّهِ وَالْيَوْمِ الْآخِرِ ، فَلْيَقُلْ خَيْرًا أَوْ لِيَصْمُتْ))   متفق عليه  .
Na kutoka kwa Abuu Hurayrah (Radhwiya Allahu 'anhu) ambaye amsema: Rasuli wa Allaah  (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((Mwenye kumuamini Allaah na siku ya Mwisho basi aseme mema au anyamaze)) [Al-Bukhaariy na Muslim]  



Ulimi ni Kufaulu kwako au Kuangamia kwako

Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Ameuhifadhi ulimi ndani ya mdomo, ili usiwe wazi kila mara ukanena maneno mengi ambayo huenda yakamuangamiza binaadamu kwa kumuharibia ‘amali zake, au kukosa radhi za Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) hata mtu akineno neno moja tu ovu ni hatari kwa sababu  Rasuli wa Allaah  (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) ameonya:

عن أبي عبد الرحمن بلال بن الْحَارِثِ الْمُزَنِيِّ رضي الله عنه أن رسول الله صلى الله عليه وسلم قال‏:‏ ((‏ان الرَّجُلَ لَيَتَكَلَّمُ بِالْكَلِمَةِ من رِضْوَانِ الله ما كان يَظُنُّ ان تَبْلُغَ ما بَلَغَتْ يَكْتُبُ الله له بها رِضْوَانَهُ إلى يَوْمِ يَلْقَاهُ وَإِنَّ الرَّجُلَ لَيَتَكَلَّمُ بِالْكَلَمِةِ من سَخَطِ الله ما كان يَظُنُّ ان تَبْلُغَ ما بَلَغَتْ يَكْتُبُ الله له بها سَخَطَهُ إلى يَوْمِ يَلْقَاهُ))‏.‏ رواه مالك في الموطأ والترمذي وقال حديث حسن صحيح‏.
Abuu 'Abdir-Rahmaan Bilaal bin Al-Haarith Al-Muzniy (Radhwiya Allaahu 'anhu) amesema: Rasuli wa Allaah  (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((Kwa hakika mja atazungumza neno linalomridhisha Allaah, wala asidhani kuwa litafikia lilipofikia, Allaah Amuandikie kwa neno hilo Radhi Zake hadi Siku ya Qiyaamah. Na Kwa hakika mja atazungumza neno linalomghadhibisha Allaah, wala asidhani kuwa litafikia lilipofikia, Allaah Amuandikie kwa neno hilo hasira Zake hadi Siku ya Qiyaamah)) [Maalik katika Muwattwa na At-Tirmidhiy ambaye amesema Hadiyth hii ni Hasan Swahiyh]

Kutokana na Hadiyth hii, tunapata funzo kwamba, ulimi unaweza kuwa ni kiungo kizuri kabisa katika mwili wa binaadamu na unaweza kuwa ni kiungo kiovu kabisa vile vile.
Kisa kifuatacho cha Luqmaan kinatuthibitishia funzo hili:

Ibn Jariyr amenukuu kwamba Khaalid Ar-Rabaai alisema: "Luqmaan alikuwa mtumwa wa Kiethiopia aliyekuwa na ujuzi wa useremala. Bwana (Tajiri) wake alimwambia: "Tuchinjie huyu kondoo." Akamchinja, kisha akamwambia: "Niletee viungo viwili vilivyokuwa ni bora kabisa." Akampelekea ulimi na moyo. Baada ya siku kupita, alimtaka tena amchinjie kondoo, akachinja kisha Bwana wake akamwambia tena: "Niletee viungo viwili vilivyokuwa ni viovu kabisa." Akameletea vile vile ulimi na moyo. Bwana wake akamuuliza: "Nilipokutaka uniletee viungo bora kabisa umeniletea ulimi na moyo; na nilipokutaka uniletee viungo viovu kabisa umeniletea hivyo hivyo." Luqmaan akamwambia: "Hakuna vilivyo bora kuliko hivi vinapokuwa vizuri, na hakuna vilivyo viovu kabisa kuliko hivi vinapokuwa vibaya." [At-Twabariy: 20:135]

Mafunzo mengineyo kuhusu ulimi:


  1. Ulimi ni kipande kidogo cha nyama kisichokuwa na mifupa lakini kinaweza kumvunja mtu mifupa yake siku ya Qiyaamah.
  1. Ulimi ni kama nyoka utakaomtia sumu binaadamu, au ni kama mkuki utakaomuangamiza binaadamu siku ya Qiyaamah.
  1. Hivyo hivyo, ulimi huenda ukawa ni sababu ya kumuingiza mtu Peponi japo kama hakuwa na matendo mengi ya wema. 

  1. Ulimi ni kiungo kikuu katika mwili wa binaadamu kinachodhibiti viungo vingine vyote vya mwili wa binaadamu kutokana na Hadiyth ifuatayo ya Rasuli wa Allaah  (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam):

عَنْ أَبِي سَعِيدٍ الْخُدْرِيِّ رَفَعَهُ قَالَ : قال رسول الله صلى الله عليه وسلم:  (( إِذَا أَصْبَحَ ابْنُ آدَمَ، فَإِنَّ الْأَعْضَاءَ كُلَّهَا تُكَفِّرُ  اللِّسَانَ، فَتَقُولُ : اتَّقِ اللَّهَ فِينَا، فَإِنَّمَا نَحْنُ بِكَ، فَإِنِ اسْتَقَمْتَ اسْتَقَمْنَا، وَإِنِ اعْوَجَجْتَ اعْوَجَجْنَا))  أخرجه الترمذي وأحمد وابن خزيمة والبيهقي بسند حسن. رياض الصالحين
Kutoka kwa Abuu Sa'iydil-Khudriyy (Radhwiya Allaahu 'anhu) kwamba Rasuli wa Allaah  (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((Anapoamka mwana Aadam viungo vyote vinaulaumu ulimi vikisema: Mche Allaah kwetu, kwani sisi tuko katika hifadhi yako; ukiimarika nasi tutaimarika, ukienda pogo, nasi tutakwenda pogo)) [At-Tirmidhiy, Ahmad, Ibn Khuzaymah, Al-Bayhaqiy ikiwa ni sanad hasan. Riyaadhwus-Swaalihiyn]

Ni vyema kuzuia ulimi usitoke kuzungumza maneno yoyote ila pale unapohitajika kwani kuuachia ulimi utamke tu ya kutamkwa bila ya kutahadhari, utampeleka mtu kutoa porojo na kuzungumza yasiyofaa na kumharibia mja Aakhirah yake.


Kuharamishwa kwake na Adhabu zake katika Quraan


Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

وَلَا تَقْفُ مَا لَيْسَ لَكَ بِهِ عِلْمٌ ۚ إِنَّ السَّمْعَ وَالْبَصَرَ وَالْفُؤَادَ كُلُّ أُولَـٰئِكَ كَانَ عَنْهُ مَسْئُولًا ﴿٣٦﴾
Na wala usifuatilie ambayo usiyokuwa nayo ujuzi. Hakika masikio na macho na moyo; vyote hivyo vitakuwa vya kuulizwa (Siku ya Qiyaamah). [Al-Israa: 36]  


Na Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

وَلَا يَغْتَب بَّعْضُكُم بَعْضًا ۚ أَيُحِبُّ أَحَدُكُمْ أَن يَأْكُلَ لَحْمَ أَخِيهِ مَيْتًا فَكَرِهْتُمُوهُ ۚ وَاتَّقُوا اللَّـهَ ۚ إِنَّ اللَّـهَ تَوَّابٌ رَّحِيمٌ﴿١٢﴾
na wala wasisengenyane baadhi yenu wengineo. Je, anapenda mmoja wenu kwamba ale nyama ya nduguye aliyekufa? Basi mmelichukia hilo! Na mcheni Allaah! Hakika Allaah ni Mwingi wa kupokea tawbah, Mwenye kurehemu. [Al-Hujuraat: 12]

Ibn 'Abbaas (Radhwiya Allaahu 'anhumaa) amesema: Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Ameharamisha Muumimi kumsengenya mwenziwe kama Alivyoharamisha nyamafu.

‘Ulamaa wamekubaliana kuwa Ghiybah ni haraam kutokana na kauli ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) iliyotangulia. Na kuhusu kauli Yake:

فَكَرِهْتُمُوهُ
((Basi mmelichukia hilo))

kwa maana kama mnavyochukia kula nyama ya ndugu yenu aliyekufa basi vile vile mchukie kumtaja mwenzenu kwa ubaya.

Anasema pia Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

وَلَا تَلْمِزُوا أَنفُسَكُمْ وَلَا تَنَابَزُوا بِالْأَلْقَابِ ۖ بِئْسَ الِاسْمُ الْفُسُوقُ بَعْدَ الْإِيمَانِ ۚ وَمَن لَّمْ يَتُبْ فَأُولَـٰئِكَ هُمُ الظَّالِمُونَ﴿١١﴾
Na wala msifedheheshane kwa kutukanana na wala msiitane majina (mabaya) ya utani. Ubaya ulioje kuita jina la ufasiki baada ya iymaan. Na yeyote asiyetubu, basi hao ndio madhalimu. [Al-Hujuraat: 11]

Mwenye kufanya hivyo; mwenye kusengenya na mwenye kumzushia mwenziwe uongo wamelaaniwa na kushutumiwa na Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) katika Aayah ifuatayo:
وَيْلٌ لِّكُلِّ هُمَزَةٍ لُّمَزَةٍ ﴿١﴾

Ole kwa kila mwenye kukebehi na kukashifu watu kwa ishara na vitendo na kwa kila mwenye kufedhehesha kwa ulimi. [Al-Humazah: 1]


Ibn 'Abbaas (Radhwiya Allaahu 'anhumaa) amesema: "Humazah ina maana yule anayetukana na kufedhehesha wenziwe." [At-Twabariy 24: 596] 

Al-Hammaaz:   Mwenye kusengenya kwa vitendo kwa mkono au kwa macho kama kukonyeza.  

Al-Lammaaz: Mwenye kusengenya kwa ulimi (kunena).

[Kauli ya Mujaahid katika Tafsiyr ya Ibn Kathiyr]

Yote hayo ni  Ghiybah na adhabu zake ni  kama zilivyotajwa katika Aayah zilizotangulia.
   
Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) kwa wanaosengenya kwa kuzulia watu maovu:

إِنَّ الَّذِينَ يُحِبُّونَ أَن تَشِيعَ الْفَاحِشَةُ فِي الَّذِينَ آمَنُوا لَهُمْ عَذَابٌ أَلِيمٌ فِي الدُّنْيَا وَالْآخِرَةِ ۚ وَاللَّـهُ يَعْلَمُ وَأَنتُمْ لَا تَعْلَمُونَ ﴿١٩﴾
Hakika wale wanaopenda uenee uchafu wa kashfa kwa wale walioamini; watapata adhabu iumizayo duniani na Aakhirah. Na Allaah Anajua nanyi hamjui. [An-Nuwr: 19].



Kuharamisihwa kwake na  Adhabu zake katika Sunnah


Makatazo na uharaam wa Ghiybah na adhabu zake katika Sunnah ni kama ifuatavyo: 


 عن أبي بكرة رضي الله عنه أن رسول الله صلى الله عليه وسلم قال في خطبته يوم النحر بمنى في حجة الوداع: ((إنَّ دِمَاءَكُمْ وَأَمْوَالَكُمْ وَأَعْرَاضَكُمْ حَرَامٌ عَلَيْكُمْ كَحُرْمَةِ يَوْمِكُمْ هَذَا فِي شَهْرِكُمْ هَذَا فِي بَلَدِكُمْ، أَلا بَلَّغْتُ؟ )) متفق عليه
Kutoka kwa Abuu Bakrah (Radhwiya Allaahu 'anhu) amesimulia  kuwa Rasuli wa Allaah  (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alisema katika khutba yake ya siku ya An-Nahr [siku ya kuchinja] huko Minaa katika  Hijjah ya kuaga: ((Hakika damu zenu, mali zenu na heshima zenu ni haraam kwenu kama uharamu (wa kutenda dhambi) siku yenu hii katika mji wenu huu. Je nimefikisha?)) [Al-Bukhaariy na Muslim]


Hadiyth hii imedhihirisha uharaam wa ghiybah yakiwemo makatazo na uharaam wa kuvunjiana heshima na kwamba ni sawa na kutenda dhambi mji mtukufu na siku tukufu hiyo ya Yawmun-Nahr (siku ya kuchinja).  


Haifai kumteta mtu hata ikiwa mtu huyo ana sifa mbaya unayoitaja madamu unaitaja nyuma yake basi huwa ni ghiybah kama  alivyosema Rasuli wa Allaah  (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam). Basi seuze iwe ni kumsengenya mtu kwa aibu asiyokuwa nayo au kumtolea aibu zake, au kumzulia kwa mabaya asiyokuwa nayo? Imeharamishwa katika Hadiyth ifuatayo:  


عن عَائِشَةَ رضي الله عنها قَالَتْ: قُلْتُ لِلنَّبِي صلى الله عليه وسلم: حَسْبُكَ مِنْ صَفِيَّةَ كَذَا وَكَذَا. فَقَالَ: ((لَقَدْ قُلْتِ كَلِمَةً لَوْ مُزِجَتْ بِمَاءِ الْبَحْرِ لَمَزَجَتْهُ)). قَالَتْ: وَحَكَيْتُ لَهُ إِنْسَانًا، فَقَالَ: ((مَا أُحِبُّ أَنِّى حَكَيْتُ إِنْسَانًا وَأَنَّ لِي كَذَا وَكَذَا))  رواه أبو داود   والترمذي   وقال: حديث حسن صحيح.

Kutoka kwa 'Aaishah (Radhwiya Allaahu 'anhaa) amesimulia: Nilimwambia Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam): "Achana na Swafiyyah; yuko kadhaa na kadhaa."  yaani ni mfupi – Rasuli wa Allaah  (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) akasema: ((Hakika umetamka neno ambalo lau lingalichanganywa na maji ya bahari yangelibadilika)) (kutokana na uvundo wa neno hilo). 'Aaishah alisema: "Siku moja nilimuigiza mtu mbele yake Rasuli wa Allaah  (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) akaniambia: ((Mimi sipendi kumuiga mtu na ilhali mimi nina kadhaa na kadhaa)) [Abu Daawuud na At-Tirmidhiy na amesema Hadiyth hii ni Hasan Swahiyh] 


Dini yetu ya Kiislam imesisitiza sana kutunziana heshima na kuhifadhiana mabaya yetu kama ilivyothibiti katika Hadiyth ifuatayo:


 عن عبد اللَّه بن عَمْرو بن الْعاص رضي اللَّه عنهما عن النَّبِيِّ صَلّى اللهُ عَلَيْهِ وسَلَّم قال  : ((الْمُسْلِمُ مَنْ سَلِمَ الْمُسْلِمُونَ مِنْ لِسانِهِ ويَدِهِ، والْمُهَاجِرُ مَنْ هَجَرَ ما نَهَى اللَّه عَنْهُ)) متفق عليه
Kutoka kwa 'Abdullaahi bin 'Amru bin Al-'Aasw (Radhwiya Allaahu 'anhumaa) ambaye amesema: Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((Muislam ni yule wanaosalimika Waislam kwa ulimi wake na mkono wake, na Muhaajir (mwenye kuhama) ni yule anayehama yale Aliyoyakataza Allaah)) [Al-Bukhaariy na Muslim]


Umuhimu wa kuhifadhi ulimi ili usimuingize mtu motoni:

عن معاذِ بن جبلٍ رضي الله عنه قال: قلت: يا رسول الله، أخْبِرني بِعَمَلٍ يُدْخِلُني الجنَةَ ويُبَاعِدُني عَنِ النارِ. قال: ((لَقَدْ سألْتَ عَنْ عَظيمٍ، وإنَهُ لَيَسيرٌ عَلى من يَسَّرَهُ اللهُ تعالى عَلَيْهِ : تَعْبُدُ اللهَ لا تُشْرِكُ بِهِ شَيئاً، وتُقيمُ الصَّلاةَ  ،وتُؤتي الزكاةَ، وتصومُ رمضانَ، وتَحُجُّ البيتَ)) ثم قال: (( ألا أَدُلُّكَ على أبْوَابِ الخيرِ؟: الصَّومُ جُنَّةٌ، والصَّدقةُ تُطْفِىءُ الخَطِيئةَ كما يُطْفىءُ الماءُ النارَ، وصَلاةَ الرَّجُلِ في جَوْفِ الَّليْلِ، ثم تلا: ((تَتَجَافَى جُنُوبُهُمْ عَنْ الْمَضَاجِعِ)) - حتى بلغ – ((يَعْمَلُونَ))  السجدة: 16-17 .
ثم قال:  ((ألا أُخْبِرُكَ بِرَأسِ الأمْرِ وَعَمودِهِ وَذِرْوَةِ سَنَامِهِ؟)) قلتُ: بَلىَ يا رسول الله. قال:  (( رَأْسُ الأمْرِ الإسلامُ، وعَمُودُهُ الصَّلاةُ، وَذِرْوَةُ سَنَامِهِ الجِهادُ )).ثم قال: ((ألا أخْبِرُكَ بِمِلاكَ ذَلِكَ  كلِّهِ ؟)) فَقُلْتُ بَلَى يا رَسول الله، فأخَذَ بِلِسانِهِ وقال:  ((كُفَّ عَلَيْكَ هذا)) . قلت: يا نبيَّ الله، وإنَّا لمؤاخَذُونَ بِما نَتَكَلَّمُ بِه؟)) فقال: (( ثَكِلَتْكَ أمُّكَ يَا مُعَاذُ،  وَهَلْ يَكُبُّ الناسَ في النارِ على وُجُوهِهِمْ ))  أو قال: ((على مناخِرِهِم - إلاَّ حَصَائدُ  ألسِنَتهم)) رَوَاهُ التِّرْمِذِيُّ   وَقَالَ: حَدِيثٌ حَسَنٌ صَحِيحٌ. 
Kutoka kwa Mu'aadh bin Jabal (Radhwiya Allaahu 'anhu) amesema: Nilisema: Ee Rasuli wa Allaah! Niambie kitendo ambacho kitanipeleka Jannah na kitaniokoa na moto.  Akasema: ((Umeniuliza jambo kubwa lakini ni rahisi kwa yule ambaye Allaah Ta’aalaa Amemsahilishia.  Muabudu Allaah wala usimshirikishe na chochote, Swali, toa Zakaah, funga Ramadhwaan, nenda kuhiji (Makka). Kisha akasema: ((Je? Nikuonyeshe  milango ya kheri?  Swawm ni ngao, Swadaqah inazima dhambi kama vile maji yanavyozima moto, na kuswali katikati ya usiku: Kisha akasoma  ((Mbavu zao zinatengana na vitanda ….)) hadi ilipomalizikia Aayah ((…waliyokuwa wakiyatenda)) [As-Sajdah: 16 na 17]  

Tena akasema: ((Je, nikwambie kilele cha hilo jambo; nguzo yake na sehemu yake ya juu kabisa?)) Nikasema: Ndio ee Rasuli wa Allaah. Akasema: ((Kilele chake ni Uislaam, nguzo yake ni Swalaah na sehemu yake ya juu kabisa ni jihaad))  Kisha akasema: ((Je, nikwambie muhimili wa yote haya?)) Nikasema: Ndio ee Rasuli wa Allaah. Akaukamata ulimi wake na akasema; ((Uzuie huu)) Nikasema: Ee Nabiy wa Allaah,  yale tunayoyasema tutahukumiwa  kwayo? Akasema:  ((Mama yako akuhurumie ee Mu'aadh!  Kuna kitu zaidi kinachowaangusha watu kifudifudi motoni kama si mavuno ya ndimi zao?)) [Imesimuliwa na At-Tirmidhiy na ni Hadiyth Hasan]


Baadhi ya hizo adhabu za Aakhirah alikwishaziona Rasuli wa Allaah  (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alipokwenda Israa wal Mi'raaj kama ilivyotajwa  katika Hadiyth ifuatayo:


عن أنس قال: قال رسول الله صلى الله عليه وسلم: ((لما عُرِجَ بي مررتُ بقومٍ لهم أظفارٌ من نُحاسٍ يخْمِشون وجوهَهم وصدورَهم، فقلتُ: من هؤلاء يا جبريلُ ؟)) قال: هؤلاء الذين يأكلون لحومِ الناسِ ، ويقعون في أعراضِهم.

Kutoka kwa Anas (Radhwiya Allaahu ‘anhu) kwamba Rasuli wa Allaah  (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((Nilipopandishwa mbinguni (Siku ya Israa na Mi’raaj) nilipita kwa watu ambao walikuwa wana kucha za shaba nyeupe wakijichana nyuso zao na vifua vyao. Nikauliza: Nani hawa ewe Jibriyl?)) Akasema: Hawa ni watu ambao wamekula nyama za binaadamu na kuwavunjia heshima zao. [Abuu Daawuwd, Swahiyh Abiy Daawuwd (4878)]



Sababu zinazopeleka katika Ghiybah 


1-Kuambatana na marafiki waovu:  


Moja ya sababu ya Ghiyba ni kuambatana na marafiki waovu wasiomkhofu Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) kwani rafiki muovu humuathiri mwenziwe kwa yale anayoyatenda. Mfano mzuri ametupigia  Rasuli wa Allaah  (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam)

عن أبي موسى الأشعري رضي الله عنه أن النبي صلى الله عليه وسلم قال: ((إِنَّمَا مَثلُ الجَلِيسِ الصَّالِحِ وَجَلِيسِ السُّوءِ كَحَامِلِ المِسْكِ وَنَافِخِ الْكِيرِ، فَحَامِلُ الْمِسْكِ إمَّا أنْ يُحْذِيَكَ وَإمَّا أنْ تَبْتَاعَ مِنْهُ وَإمَّا أنْ تَجِدَ مِنْهُ ريحًا طَيِّبَةً، وَنَافِخُ الكِيرِ إمَّا أنْ يُحْرِقَ ثِيَابَكَ وَإمَّا أنْ تَجِدَ مِنْهُ رِيحًا مُنْتِنَةً )) متفق عليه
Abuu Muwsaa Al-Ash'ariyy (Radhwiya Allaahu 'anhu) amesimulia: Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((Mfano wa rafiki mwema unayeambatana naye rafiki  mbaya ni kama mfano wa mbebaji miski na mfua chuma (anayevuvia kipulizo). Mbebaji miski ima atakupa au utanunua kutoka kwake au utapata harufu nzuri kwake. Na mfua chuma (anayepuliza kipulizo), ima atachoma nguo zako au utapata harufu mbaya kutoka kwake)) [Al-Bukhaariy na Muslim]


2-Mwenye kusengenya kutokuzingatia aibu zake:    

Ghiybah ni maasi yanayoleta madhara makubwa baina ya ndugu wa Kiislamu kwa kukashifiana na kutangaziana aibu zao. Tutambue kuwa hakuna mwana Aadam aliyekamilika, na kila mtu atakuwa na aibu zake; kama si aibu yake mwenyewe, basi huenda ikawa kuna aibu katika familia yake, na kama si familia yake basi huenda akawa ni mtu wa karibu yake n.k.  Na hata kama hakuna aibu yoyote kwake au kwa watu wake, basi akhofu kuwa huenda ikamfikia yeye aibu hiyo au ndugu zake au watoto wake au yeyote katika jamaa zake, kwa sababu huenda Allaah Akalipizia hapa hapa duniani kwa wenye kusengenya kwa kuwasibu nao yatakayopelekea watu kuwasengenya.


3-Simu ni chanzo kikuu:

Chanzo kikuu kinachofanikisha kutendeke Ghiybah na uzushi kuenea katika jamii kwa siku hizi ni simu, hasa kwa kuweko mawasiliano ya bure kama mitandao ya kijamii.    Lau kama simu zingelikuwa ni za kulipiwa basi bila shaka wangelifilisika wenye kupenda kusengenya na kuzusha.  


4-Kudhani kwamba kusikiliza umbeya, uzushi, hakuhusiani na  ghiybah:


Mara nyingi utamsikia mtu anasema: "Lakini mimi nasikiliza tu sitii langu!” Mwenye kusema hivi atambue kuwa mwenye kusengenya na mwenye kusikia wote wako katika ushirikiano wa maasi haya ya ghiybah. Na kila kiungo cha mwana Aadam kitamchongea mwenye kufanya maasi siku ya Qiyaamah, hivyo masikio yatakuchongea unaposikiliza umbeya au usengenyaji kwani Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Anasema:

إِنَّ السَّمْعَ وَالْبَصَرَ وَالْفُؤَادَ كُلُّ أُولَـٰئِكَ كَانَ عَنْهُ مَسْئُولًا ﴿٣٦﴾
Hakika masikio na macho na moyo; vyote hivyo vitakuwa vya kuulizwa (Siku ya Qiyaamah).  [Al-Israa: 36]


5-Kujishughulisha na upuuzi badala ya kutumia muda kwa mambo yenye manufaa ya Dini:


Kuwa na faragha (muda na wasaa) ni neema ambayo inampasa Muislamu ashukuru, kwani kila dakika  ni muhimu kuitumia ipasavyo  kwa kujichumia mema na sio kuipoteza kwa mambo ya upuuzi ambayo yanayoweza kumuamgamiza mtu motoni kama Anavyosema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

فَوَيْلٌ يَوْمَئِذٍ لِّلْمُكَذِّبِينَ ﴿١١﴾
Basi ole Siku hiyo kwa wakadhibishao.

الَّذِينَ هُمْ فِي خَوْضٍ يَلْعَبُونَ ﴿١٢﴾
Ambao wamo katika kushughulika na upuuzi wakicheza.         [At-Twuwr: 11-12]


Amesema Imaam Ibn Kathiyr: "Ni wale ambao duniani wanacheza katika mambo ya batili."  Na kusengenya ni maovu, dhambi na batili inayompasa Muislamu ajiepushe nayo.



Namna ya Kujiokoa na Kuokoa Jamii kutokana na Ghiybah


Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

وَإِذَا رَأَيْتَ الَّذِينَ يَخُوضُونَ فِي آيَاتِنَا فَأَعْرِضْ عَنْهُمْ حَتَّىٰ يَخُوضُوا فِي حَدِيثٍ غَيْرِهِ ۚ وَإِمَّا يُنسِيَنَّكَ الشَّيْطَانُ فَلَا تَقْعُدْ بَعْدَ الذِّكْرَىٰ مَعَ الْقَوْمِ الظَّالِمِينَ ﴿٦٨﴾
Na unapowaona wale wanaoshughulika kupiga porojo katika Aayaat Zetu; basi jitenge nao mpaka watumbukie kwenye mazungumzo mengineyo. Na kama shaytwaan akikusahaulisha, basi baada ya kukumbuka, usikae pamoja na watu madhalimu. [Al-An'aam: 68]


Hiyo ni moja ya njia ya kujiokoa na maovu haya ya Ghiybah, nayo ni kujiepusha na wanaopendelea kuzungumza yasiyo na maana na yanayomkosesha mtu radhi za Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa). Njia nyingine nyingi ni kama yafuatayo:


Njia Za Kujiokoa Na Kuwaokoa Wenzako Na Ghiybah:

1.  Kuwa na taqwa na umkhofu Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa)  na kusoma Aayah na Hadiyth zenye maonyo na adhabu za Ghiybah.

2. Kufikiria khasara utakayopata kuporomoka ‘amali zako njema zote na badala yake kujazwa madhambi   kama inavyosema Hadiyth ifuatayo:


‏ ‏عن ‏ ‏أبي هريرة رضي الله عنه  أَنَّ رَسُولَ اللَّهِ صَلَّى اللَّهم عَلَيْهِ وَسَلَّمَ قَالَ: ((أَتَدْرُونَ مَا الْمُفْلِسُ)) قَالُوا: الْمُفْلِسُ فِينَا مَنْ لا دِرْهَمَ لَهُ وَلا مَتَاعَ، فَقَالَ: ((إِنَّ الْمُفْلِسَ مِنْ أُمَّتِي يَأْتِي يَوْمَ الْقِيَامَةِ بِصَلاةٍ وَصِيَامٍ وَزَكَاةٍ وَيَأْتِي قَدْ شَتَمَ هَذَا وَقَذَفَ هَذَا وَأَكَلَ مَالَ هَذَا وَسَفَكَ دَمَ هَذَا وَضَرَبَ هَذَا فَيُعْطَى هَذَا مِنْ حَسَنَاتِهِ وَهَذَا مِنْ حَسَنَاتِهِ فَإِنْ فَنِيَتْ حَسَنَاتُهُ قَبْلَ أَنْ يُقْضَى مَا عَلَيْهِ أُخِذَ مِنْ خَطَايَاهُمْ فَطُرِحَتْ عَلَيْهِ ثُمَّ طُرِحَ فِي النَّارِ)) مسلم، الترمذي
Imetoka kwa Abuu Hurayrah (Radhwiya Allaahu 'anhu) kwamba Rasuli wa Allaah  (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((Mnamjua nani aliyefilisika?)) Wakasema (Maswahaba): Aliyefilisika ni yule miongoni mwetu asiyekuwa na dirham au mali. Rasuli wa Allaah  (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) akasema: ((Aliyefilisika katika Ummah wangu ni yule atakayekuja siku ya Qiyaamah na Swalaah zake, Swawm zake na Zakaah zake, lakini atakuja akiwa amemtukana huyu, amemtuhumu huyu, amekula mali ya huyu, amemwaga damu ya huyu na amempiga huyu, yatachukuliwa mema yake na kulipwa wale aliowadhulumu. Yatakapomalizika mema yake kabla ya kufidia madhambi aliyowakosea wenzake, zitachukuliwa dhambi za wale aliowakosea kisha atajaziwa yeye na mwishowe atakuwa ni wa kutupwa motoni)) [Muslim, At-Tirmidhiy]


3.  Fikiria aibu zako au aibu za ndugu, jamaa zako na uwaze kama utapenda aibu hizo zidhihirike kwa wengine.


4.  Mshukuru Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) kwa kukuepusha na aibu kama za wenzako na muombe Asikupe mtihani wa aibu kama hizo au nyinginezo.


5.  Jiepushe na watu waovu na vikao viovu na andamana na watu wema ambao watakuwa na mazungumzo ya kukupa faida badala ya kukuangamiza.


6. Atakapokutafuta mwenzio kutaka kusengenya, muelezee wazi kuwa hutaki tena kusikia umbeya kwani unamkhofu Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa), na umnasihi naye pia aache maouvu hayo kwa kumkumbusha adhabu zake.


7. Jipe adhabu mwenyewe kila unapomsengenya mtu kama walivyokuwa wakifanya Salafus-Swaalih (wema waliotangulia);

-Funga Swawm ya siku moja kila unapomsengenya mtu, hatimaye utashindwa kukaa na njaa kila siku.

-Toa kiasi fulani cha pesa kila unapomsengenya mtu, utakapojiona unafilikisha utaacha kusengenya. 


8. Hifadhi ulimi wako usizungumze ila mema tu, jifunze pole pole hata kwa kujikumbusha, mfano uweke kitu mdomoni kama kijiwe au chembe ngumu isiyotafunika ili ibakie kukukumbusha kuzuia ulimi kusema yasiyo na maana.

9. Jiepushe na moto pindi utakapolinda heshima ya mwenzio, kumbuka Hadiyth ifuatayo:

عن أبي الدرداء رضي الله عنه عن النبي صلى الله عليه وسلم قال: ((مَنْ رَدَّ عَنْ عِرْضِ أَخِيهِ رَدَّ اللهُ عَنْ وَجْهِهِ النَّارَ يَوْمَ الْقِيَامَةِ)) رواه الترمذي وحسنه

Abuu Ad-Dardaa (Radhwiya Allaahu 'anhu) amesema: Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((Atakayetetea heshima ya nduguye (Muislamu), Allaah Atamuepusha uso wake na moto)) [At-Tirmidhiy na amesema Hadiyth hii ni Hasan]


10.           Utakaposikia uzushi, kashfa au mtu atakapomsengenya mwenziwe mbele yako sema kama Anavyotufunza Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) katika Aayah zifuatazo kuhusu kisa cha 'ifk' (uzushi wa kusingiziwa Mama wa Waumimi 'Aaishah Radhwiya Allaahu 'anhaa):


Kwanza: Jifikirie nafsi yako kama wewe pia unaweza kufanya maovu hayo yanayozungumzwa? Kwa hiyo uweke dhana nzuri pia kwa Waumini wenzako.


لَّوْلَا إِذْ سَمِعْتُمُوهُ ظَنَّ الْمُؤْمِنُونَ وَالْمُؤْمِنَاتُ بِأَنفُسِهِمْ خَيْرًا وَقَالُوا هَـٰذَا إِفْكٌ مُّبِينٌ ﴿١٢﴾
Kwa nini mlipoisikia (kashfa ya kusingiziwa), Waumini wanaume na Waumini wanawake wasiwadhanie wenzao kheri, na wakasema: “Hii ni kashfa ya kusingizwa iliyo dhahiri?”[An-Nuwr: 12]


Pili:  Kanusha kabisa uliyoyasikia na chukulia hayo kuwa ni uzushi na Msabbih Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):   
وَلَوْلَا إِذْ سَمِعْتُمُوهُ قُلْتُم مَّا يَكُونُ لَنَا أَن نَّتَكَلَّمَ بِهَـٰذَا سُبْحَانَكَ هَـٰذَا بُهْتَانٌ عَظِيمٌ ﴿١٦﴾
Na kwa nini mlipoisikia (kashfa ya kusingiziwa) msiseme: “Haitupasi sisi tuzungumze haya; Subhaanak! (Utakasifu ni Wako) huu ni usingiziaji wa dhulma mkubwa mno!” [An-Nuwr: 16]



Kafara (Fidia) Ya Ghiybah


Ghiybah ni madhambi ambayo yanayomharibia mtu ‘amali zake njema na badala yake ni kujazwa dhambi za yule anayemsengenya na hatimaye kumuangamiza motoni. Hivyo inampasa Muislamu mwenye tabia hii ovu ambayo ni hatari kwake, afanye haraka kafara ya maovu hayo kama ifuatavyo:


1-Tawbah (Kutubia)

Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):
 يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا تُوبُوا إِلَى اللَّـهِ تَوْبَةً نَّصُوحًا
  Enyi walioamini! Tubieni kwa Allaah tawbah ya nasuha (kwelikweli) [At-Tahriym: 8]


Tawbatun-Naswuwhaa (Tawbah ya kweli) ni ile mtu anayokamilisha shuruti zake nazo ni:


  • Kuacha kitendo kiovu hicho.
  • Kujuta
  • Kuazimia kutokurudia tena maovu
  • Ikiwa inahusu haki ya binaadamu basi lazima kwanza kurudisha haki hiyo.

2-Vipi ujihalalishe na Ghiybah

Kama ilivyo sharti ya nne kuwa kwa vile Ghiybah inahusu haki ya binaadamu basi lazima kwanza urudishe haki ya uliyemsengenya hapa duniani kabla ya kuhesabiwa Aakhirah, kwani Hadiyth ifuatayo inatuelezea,


عن أبي هريرة رضي الله عنه عن النبي صلى الله عليه وسلم  قال: ((من كانت عنده مظلمة لأخيه من عرضه أو من شيء، فليتحلله منها اليوم قبل أن لا يكون دينار ولا درهم، إن كان له عمل صالح أخذ منه بقدر مظلمته، وإن لم يكن له حسنات أخذ من سيئات صاحبه فحمل عليه  [رواه البخاري

Kutoka kwa Abu Hurayrah (Radhwiya Allaahu 'anhu) ambaye amesimulia kwamba: Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((Mwenye kitu cha dhulma cha nduguye kutokana na kumvunjia heshima au kitu chochote, basi amuombe amhalalishie leo kabla haijafika siku ambayo hakutakuwa na dinari wala dirhamu; akiwa ana amali njema itachukuliwa kwa kadiri ya alichodhulumu, na akiwa hana amali njema, zitachukuliwa dhambi za aliyemdhulumu na abebeshwe)) [Al-Bukhaariy]

عَنْ أَبِي هُرَيْرَةَ (رضي الله عنه) عَنْ النَّبِيِّ (صلى الله عليه و آله وسلم) قَالَ:  ((مَنْ كَانَتْ عِنْدَهُ مَظْلَمَةٌ مِنْ أَخِيهِ مِنْ عِرْضِهِ أَوْ  مِنْ شَيْءٍ  فَلْيَتَحَلَّلْهُ مِنْهُ الْيَوْمَ قَبْلَ أَنْ لاَ يَكُونُ دِينَارٌ وَلاَ دِرْهَمٌ ، وَإِنْ كَانَ لَهُ عَمَلٌ صَالِحٌ أُخِذَ مِنْهُ بِقَدْرِ مَظْلَمَتِهِ. وَإِنْ لَمْ يَكُنْ لَهُ أُخِذَ مِنْ سَيِّئَاتِ صَاحِبِهِ فَحُمِل عَلَيْهِ))  رواه البخاري
Imepokelewa kutoka kwa Abuu Hurayrah (Radhwiya Allaahu 'anhu)  kwamba Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((Aliyekuwa na kitu cha dhulma cha nduguye kutokana na kumvunjia heshima au kitu chochote, basi amuombe amhalalishie leo kabla haijafika siku ambayo hakutakuwa na dinari wala dirham. Ikiwa ana ‘amali njema, basi zitachukuliwa kwa kadiri ya alichodhulumiwa. Na ikiwa hana, basi zitachukuliwa dhambi za aliyemdhulumu abebeshwe)). [Al-Bukhaariy]


3-Mwenye kusengenywa asiwe na huzuni kwa kufanyiwa maovu haya kwani ni yeye mwenye kufaidika kwa kuchuma mema ambayo hakutia juhudi zake zozote za kuzifanyia kazi.  


Inasemekana kuwa Hasan Al-Baswry alimpelekea zawadi mtu aliyemsengenya na kumshukuru kwa kumchumia amali ambazo hakuzifanyia kazi kabisa.


4-Tutazame kauli zifuatazo za Salaf kuhusu kujihalalisha na Ghiybah:


- Sufyaan bin 'Uyaynah amesema: "Ghiybah ni dhambi kubwa kwa Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) kuliko zinaa au kunywa pombe kwani hizo ni dhambi baina ya mja na Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa), utakapotubu Atakughufuria, lakini Ghiybah ni baina ya mja na nduguye hadi amsamehe."

Kama tunavyojua kuwa ni vigumu sana mtu kuwa na moyo wa kumsamehe mwenzake anapomsengenya, ndio maana labda Salaf huyu akaona kuwa kusengenya ni madhambi makubwa zaidi kuliko madhambi mengine makubwa.


- Ibn Taymiyah, Ibnul Qayyim na wengineo, wameona kuwa sharti ya kujihalalisha na Ghiybah inaanguka pindi ukihisi kuwa utaharibu uhusiano wa uliyemsengenya na kuzidisha chuki na uadui baina yenu.


5-Sio wepesi kwa mtu mwenye kusengenya kumfuata mwenziwe na kumuomba msamaha kwa khofu ya kuwa ataharibu uhusiano. 

Hali kadhalika sio wepesi kwa mwenye kusengenywa kusamehe, kwani ni jambo linalomuumiza mtu moyoni khaswa ikiwa aliyekusengenya ni rafiki yako mpenzi au mtu wa karibu yako. 

Pindi hali ikiwa ni hivyo ya kusababisha chuki, uadui na kutoweka mapenzi na masikilizano, ni bora kutokumuomba msamaha bali fanya yafuatayo:


  • Muombee maghfirah kwa Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Amghufurie madhambi yake.
  • Muombee du'aa za kumtakia kheri nyingi duniani na Aakhirah.
  • Mfanyie wema kwa wingi.  

Tunamuomba Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Atuepushe na maovu haya tusifike hadi hali zetu zikawa za kujuta na khasara ya kupoteza ‘amali zetu tunazojitahidi kuzifanya duniani kumbe hatuzimiliki Aakhirah.


Hali zinazoruhusu Ghiybah


Tumebainishiwa katika Shariy’ah yetu ya Kiislamu kuwa ziko hali zinazojuzu  Ghiybah kwa sababu ya maslaha yanayopatikana. Nazo ni kama ifuatavyo:



1-Kupinga dhulma ya Qadhi au Kiongozi au kuzuia dhulma isitendeke:

Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):
 لَّا يُحِبُّ اللَّـهُ الْجَهْرَ بِالسُّوءِ مِنَ الْقَوْلِ إِلَّا مَن ظُلِمَ
Allaah Hapendi uovu utajwe hadharani isipokuwa kwa yule aliyedhulumiwa. [An-Nisaa: 148].  


2-Katika kushitaki anapodhulumiwa mtu haki yake:

Kutoa aibu ya mtu inapohitajika mfano kushtaki kwa mhusika (mkuu atakayeweza kutatua matatizo) mfano kulalamika: “Fulani kanidhulumu kadhaa na kadhaa, au kanifanyia kadhaa na kadhaa, au fulani hanipi haki yangu kadhaa na kadhaa."  Hii ni kutokana na dalili ifuatayo:


عَنْ عَائِشَةَ، أَنَّ هِنْدَ بِنْتَ عُتْبَةَ، قَالَتْ : يَا رَسُولَ اللَّهِ إِنَّ أَبَا سُفْيَانَ رَجُلٌ شَحِيحٌ وَلَيْسَ يُعْطِينِي مَا يَكْفِينِي وَوَلَدِي، إِلَّا مَا أَخَذْتُ مِنْهُ وَهُوَ لاَ يَعْلَمُ، فَقَالَ: ((خُذِي مَا يَكْفِيكِ وَوَلَدَكِ ، بِالْمَعْرُوفِ )) متفق عليه
Kutoka kwa 'Aaishah (Radhwiya Allaahu 'anhaa) kwamba Hind mke wa Abuu Sufyaan alisema: "Ee Rasuli wa Allaah , Hakika Abuu Sufyaan ni mtu bakhili, wala hanipi kinachonitosha mimi na mwanangu ila ninachokichukua ilihali hajui." (ni sawa hivi nifanyavyo?) Rasuli wa Allaah  (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) akamwambia: ((Chukua kwa wema kinachokutosha wewe na mwanao)) [Al-Bukhaariy na Muslim]


3-Katika hali ya kubadilisha maovu:

Huenda Muislamu akaona maovu yanatendeka na hatoweza kuyaondosha ila aulizie sababu, na huenda atakayeulizwa amseme aliyetenda maovu mfano kusema: “Fulani ndiye aliyefanya ovu hili kadhaa na kadhaa."


4-Kujikinga na shari, na kunapotolewa nasiha kwa Waislamu:

عنْ فاطِمَة بِنْت قَيْس رضي الله عنها قالت أتَيْت النبي صلى الله عليه وسلم فَقُلْتُ إنَّ أبا الجهم ومعاوية خطباني فقال رسول الله صلى الله عليه وسلم ( أَمَّا مُعَاوِيَةُ فَصُعْلُوكٌ لَا مَالَ لَهُ، وَأَمَّا أَبُو جَهْمٍ فَلَا يَضَعُ عَصَاهُ عَنْ عَاتِقِهِ)) )) متفق
وفي رواية لمسلم ((وأما أبو الجهم فضراب للنساء)) وهو تفسير لرواية لا يضع العصا عن عاتقه وقيل معناه كثير الأسفار
Faatwimah binti Qays (Radhwiya Allaahu 'anhaa) amesimulia: "Nilimuendea Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) nikamuambia: "Abul-Jahmi na Mu'aawiyah wameniposa." Rasuli wa Allaah (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) akaniambia: ((Ama Mu'aawiyah ni mtu fukara hanamali. Ama Abul-Jahmi haondoi fimbo juu ya shingo yake)) [Al-Bukhaaariy na Muslim]

Katika Riwaayah nyingine ya Muslim imesema: ((Na ama Abul-Jahmi anawapiga mno wanawake))

Riwaayah hii ni tafsiyr ya riwaayah isemayo: ((…haondoi fimbo juu ya shingo yake)) Na pia imesemekana kuwa maana ya kutoondosha fimbo juu ya shingo yake ni kuwa, anasafiri mno.

Ibn Taymiyyah amesema: Huenda anapotajwa kwa ubaya mtu kukawa ni kwa ajili ya nasiha kwa Waislamu kwa usalama au manufaa ya Dini yao na dunia yao.


5-Kuwasengenya mafisadi na watu wenye shaka:

Kama ilivyo katika Hadiyth ifuatayo ambayo Al-Bukhaairy ametoa hoja kuwa Hadiyth hii yafaa kuwasengenya mafisadi na watu wenye shaka.

عن عَائِشَةَ رَضِيَ اللَّهُ عَنْهَا أن رَجُلاً اسْتَأْذَنَ عَلَى النبي صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ فَقَالَ: ((ائْذَنُوا لَهُ بِئْسَ أَخُو الْعَشِيرَةِ))  متفق

Kutoka kwa 'Aaishah (Radhwiya Allaahu 'anha) amesimulia kuwa mtu mmoja aliomba idhini ya kuingia kwa Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) akasema: ((Mruhusuni, ni mtu mbaya katika kabila lake)) [Al-Bukhaariy na Muslim]

6-Kuihami Dini kutokana na wanafiki:

عن عائشة رضي الله عنها قالت قال رسول الله صلى الله عليه وسلم ((مَا أَظُنُّ فُلاَنًا وَفُلاَنًا يَعْرِفَانِ مِنْ دِينِنَا شَيْئًا))   رواه البخاري
قال الليث بن سعد أحد رواة هذا الحديث كَانَا رَجُلَيْنِ مِنَ المُنَافِقِينَ 
Kutoka kwa 'Aaishah (Radhwiya Allaahu 'anhaa) amesema: Rasuli wa Allaah  (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((Sidhani fulani na fulani wanajua chochote katika Dini yetu)) [Al-Bukhaariy]

Layth bin Sa'ad ambaye ni mmoja wa wapokezi wa Hadiyth hii amesema: "Watu hawa wawili walikuwa ni katika wanafiki."

NA  ALLAAH ANAJUA  ZAIDI


from fisabilillaah.com https://ift.tt/2PAOgGg
via IFTTT

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

20-Hakika Shirki Ni Dhulma Kubwa Mno! - Isti’aadhah Kwa Asiyekuwa Allaah

  إِنَّ الشِّرْكَ لَظُلْمٌ عَظِيم   Hakika Shirki Ni Dhulma Kubwa Mno!   20 - Isti’aadhah  (Kuomba Kinga) Kwa Asiyekuwa Allaah   ...